Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Ali Mohamed Shein akiwapungia wananchi
baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Amaan kuhudhuria sherehe za Mapinduzi
Matukufu ya Zanzibar mjini Unguja jana.
RAIS wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein amewataka wananchi wa
Zanzibar, kulinda na kuenzi Mapinduzi ya Januari mwaka 1964 kwa nguvu
zote.
Amesisitiza kuwa mapinduzi hayo, ndiyo kielelezo cha utu wa Mwafrika
kuheshimika na kuwa huru katika nchi yake. Dk Shein alisema hayo katika
kilele cha sherehe za miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar, zilizofanyika
katika Uwanja wa Amaan mjini hapa.
Sherehe hizo zilihudhuriwa na viongozi wa kitaifa, akiwemo Rais wa
Muungano, John Magufuli na wananchi wa mikoa mitano ya Unguja na Pemba.
Alisema wananchi wa Zanzibar wanayo kila sababu ya kusherehekea na
kuadhimisha Mapinduzi ya Zanzibar, kwani matunda yake yamewanufaisha
wananchi wote bila ya kubagua.
Alisema malengo ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964, ambayo
yaliwafanya waasisi kufanya Mapinduzi, yanaendelea kutimizwa na
kutekelezwa kwa vitendo katika sekta mbali mbali muhimu, ikiwemo elimu
na sekta ya afya.
Huduma za afya
Rais Shein ambaye alitumia muda mrefu kuelezea mafanikio
yaliyopatikana katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, alisema sekta
ya afya imepata mafanikio makubwa, ikiwemo kufuta ada zilizokuwa
zikitozwa kwa wajawazito wakati wa kujifungua katika hospitali za
serikali.
Alisema hatua hiyo imesaidia mno, ambapo mwaka 2014/2015 idadi ya
wanaojifungua katika hospitali za serikali imefikia asilimia 67.8 kutoka
asilimia 56.1 katika mwaka 2013.
“Haya ni mafanikio makubwa ambayo yanakwenda moja kwa moja na malengo
yetu ya kupambana na vifo vya akinamama vinavyotokana na uzazi na
kuwafanya akinamama wote kujifungua na kupata huduma kutoka kwa
wataalamu wanaotambuliwa,” alisema.
Alisema SMZ hivi sasa imefuta gharama zote zilizokuwa zikitolewa za
kuchangia matibabu katika hospitali kuu za serikali kwa vipimo vya
uchunguzi wa maradhi mbali mbali.
Hatua hiyo imeimarisha huduma za afya katika hospitali kuu za
serikali, ikiwemo ya Abdalla Mzee iliyopo Pemba, ambayo ujenzi wake
utakapomalizika mwaka huu, itakuwa na hadhi ya rufaa.
“Ujenzi wa hospitali ya Abdalla Mzee unaofanywa na marafiki zetu wa
China, ukimalizika utaifanya kuwa na hadhi ya rufaa kwa kutoa huduma za
tiba zote ikiwemo upasuaji wa aina mbali mbali,” alisema.
Sekta ya elimu
Alisema sekta ya elimu imepata mafanikio makubwa mara baada ya
mapinduzi ya mwaka 1964. Shule za maandalizi zimefikia 270, wakati shule
za msingi kwa mwaka jana, zimefika 370.
Shein alisema idadi ya shule za sekondari, imeongezeka kutoka 210
hadi kufikia 263 huku serikali ikiweka mkazo zaidi katika ujenzi wa vyuo
vya amali. Vitajengwa Makuchuchi na Mtambwe katika mwaka ujao wa fedha
kutokana na Mkopo wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).
Mambo mengine yaliyofanywa ni serikali kutilia mkazo ujenzi wa vyuo
vya amali kwa ajili ya kuwezesha wahitimu wake kuwa na ujuzi,
utakaowafanya kujiajiri moja kwa moja. Utunzaji mazingira Aidha Shein
aliwataka wananchi kupambana na vitendo vya uharibifu wa mazingira
vinavyokwenda sambamba na mabadiliko ya tabia ya nchi.
Alisema serikali imechukua juhudi za makusudi ikiwemo kuundwa kwa
mamlaka ya usimamizi wa mazingira kukabili athari zinazojitokeza ikiwemo
za ukataji miti.
Alisema miti aina ya mikoko milioni 50, inatarajiwa kuoteshwa kwa
ajili ya kukabili athari za mazingira na kuzuia kasi ya maji ya bahari
kuvamia maeneo ya nchi kavu.
Pensheni kwa wazee
Kuhusu mikakati ya kutunza wazee wasiojiweza, Dk Shein alisema moja
ya malengo ya mapinduzi ya mwaka 1964 ni kuona wazee wanalindwa na
kuenziwa.
Alitoa mfano wa Rais wa Kwanza wa Zanzibar, Abeid Amaan Karume aliyeamua kujenga makazi ya kudumu eneo la Sebleni na Pemba.
Alisema katika mwaka wa fedha 2016, serikali ipo katika hatua za
mwisho za kusajili wazee waliostaafu, ambao watakuwa wakilipwa fedha za
pensheni ya jamii kwa wazee waliofikia umri wa miaka 70.
Jumla ya wazee 22,243 wamesajiliwa kwa ajili ya malipo ya pensheni
huku serikali ikiwa imetenga Sh milioni 20 kwa ajili ya kupunguza makali
ya ugumu wa maisha kwa wazee wastaafu wote waliofikia umri wa miaka 70.
Hali ya kisiasa
Kuhusu hali ya kisiasa Zanzibar ambayo imetokana na kufutwa kwa
uchaguzi mkuu wa Oktoba 25 mwaka jana, Dk Shein aliwataka wananchi kuwa
watulivu.
Aliwahakikishia kwamba mazungumzo ya kusaka suluhu yanayowahusisha
viongozi waliopo serikalini na wastaafu, yanaendelea vizuri. Uchaguzi wa
Oktoba 25 ulifutwa na Tume ya Uchaguzi wa Zanzibar (ZEC) na kutangazwa
katika gazeti rasmi la serikali la Novemba 6 mwaka jana.
“Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 na Sheria ya Uchaguzi Namba 11 ya
mwaka 1984, ndiyo inayosimamia uchaguzi chini ya Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar ( ZEC) kwamba uchaguzi huo umefutwa...Tume ya uchaguzi
itatangaza tarehe nyingine ya kurudiwa kwa uchaguzi huo,” alisema Shein.
Aliwapongeza wananchi kwa kudumisha amani na utulivu katika kipindi
chote; hatua aliyosema imeifanya Zanzibar kupiga hatua kubwa ya
maendeleo ya kiuchumi na uwekezaji wa sekta mbali mbali na kupokea
watalii kama kawaida. Oktoba 28 mwaka jana, Mwenyekiti wa Tume ya
Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha, alitoa “Taarifa Kwa Umma
ya Kufuta Uchaguzi wa Zanzibar”.
Katika taarifa hiyo, Jecha Salim Jecha alisema “Mimi nikiwa
Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, nimeridhika kwamba uchaguzi
huu haukuwa wa haki na kuna ukiukwaji mkubwa wa Sheria na taratibu za
uchaguzi. Hivyo, kwa uwezo nilionao natangaza rasmi kwamba uchaguzi huu
na matokeo yake yote yamefutwa na kwamba kuna haja ya kurudia uchaguzi
huu”.
Jecha alitaja sababu zilizosababisha kufutwa kwa uchaguzi huo wa
Zanzibar kuwa ni: Baadhi ya vituo vya uchaguzi katika Kisiwa cha Pemba
kuwa na idadi kubwa ya kura, zilizopigwa kuliko idadi ya watu waliopo
katika Daftari la Wapiga Kura.
Sababu nyingine ni kadi za kupigia kura hazijachukuliwa, lakini watu
wamepiga kura. Jecha alisema sababu nyingine ni kuvamiwa kwa vituo vya
kupigia kura na kuibuka kwa fujo na kusababisha watu wengine kushindwa
kupiga kura.
Fujo katika vituo vya kupigia kura zilijitokeza katika majimbo
yaliyopo kisiwa cha Pemba, ikiwemo Micheweni, Tumbe na Konde. Alitaja
sababu nyingine ni vyama vya siasa kuingilia mchakato na kazi za Tume ya
Uchaguzi na hatimaye baadhi ya vyama, kujitangazia ushindi katika
uchaguzi huo, ikiwa ni kinyume cha sheria za Tume ya Uchaguzi.
Alisema uamuzi wa kutangaza matokeo ya urais kinyume cha sheria za
Tume ya Uchaguzi ni hatari na ungeweza kuliingiza taifa katika
machafuko.
Januari 12 kila mwaka ni maadhimisho ya mapinduzi ya mwaka 1964,
ambayo yaling’oa utawala wa sultani kutoka Oman na wananchi wazalendo
walio wengi kushika hatamu ya uongozi.
Mapinduzi hayo yaliongozwa na Rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amaan
Karume, ambaye mwaka 1972 Aprili aliuawa na wapinga maendeleo, ikiwa ni
sehemu ya jaribio la kupindua utawala uliokuwa ukiongozwa na chama cha
Afro Shiraz (ASP), ambacho mwaka 1977 kiliungana na TANU kuanzisha CCM.
Rais Magufuli ashangiliwa
Mamia ya wananchi wa mikoa mitano ya Unguja, walijitokeza kwa wingi
katika Uwanja wa Amaan, kusherehekea miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Maandamano ya wananchi hao wa mikoa mitano ya Unguja, yalipita mbele ya
mgeni rasmi Rais wa Zanzibar, Dk Shein na wageni mashuhuri.
Ngoma ya asili za watu wa Unguja na gwaride la vikosi vya ulinzi,
vikiongozwa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), vilipamba
sherehe hizo. Wananchi walianza kuingia uwanjani kuanzia saa 1 asubuhi.
Baadaye umati wa watu ulifurika huku wengine wakilazimika kubaki nje ya
uwanja.
Meli ya Mv Mapinduzi ililazimika kusafirisha wananchi kutoka Kisiwa cha Pemba kuhudhuria sherehe hizo.
‘Yadumu mapinduzi ya Januari 1964’ ni maneno yaliyoandikwa katika
baadhi ya mabango, yaliyobebwa na waandamanaji waliopita mbele ya mgeni
rasmi. Rais John Magufuli alishangiliwa kwa nguvu na wananchi alipoingia
uwanjani hapo na kupigiwa wimbo wa taifa.
“Hapa Kazi Tu” ni kauli zilizosikika kutoka kwa wananchi katika
uwanja huo, ambapo ni mara ya kwanza kwa Magufuli kuhudhuria sherehe
hizo za kitaifa za Mapinduzi, akiwa Rais wa Muungano.
Chanzo Gazeti la HabariLeo.
Wednesday, 13 January 2016
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment