Thursday, 14 January 2016

Tagged Under:

Chadema wahimizwa kumuunga mkono Rais Magufuli122,4

By: Unknown On: 00:49
  • Share The Gag
  • Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa, Itikadi na Uenezi CCM, Nape Nnauye
    CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) imekitaka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), endapo kina nia ya dhati ya kupambana na ufisadi, kijitangaze hadharani kumuunga mkono Rais John Magufuli katika vita hiyo na si kuudanganya umma.
    Pia imekitaka chama hicho ili kitekeleze vyema na kuibeba ajenda hiyo ya ufisadi, kiwafukuze wanachama wake, wanaotuhumiwa kwa rushwa.
    Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa, Itikadi na Uenezi CCM, Nape Nnauye aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari, ambapo alijibu hoja ya Mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu aliyedai kuwa ajenda ya ufisadi inayotekelezwa kwa vitendo na Dk Magufuli, ni ya chama122,4 hicho na ni ya kudumu.
    Nape ambaye pia ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, alisema Lissu ameudanganya umma wa Watanzania kwa kuwa anafahamu fika kuwa chama chake kilishajiengua na ajenda tangu kipindi cha Uchaguzi Mkuu mwaka jana.
    “Lissu anadai eti ajenda ya kupiga vita ufisadi ni ya chama chao, kauli hii inashangaza kwa sababu kipindi cha kampeni Chadema ilijitenga kabisa na ajenda ya ufisadi tena si tu kuizungumzia, walijitenga nayo hata kwa vitendo,” alisisitiza Nape ambaye alikuwa mstari wa mbele ndani ya chama chake kupinga mafisadi.
    Alisema kama kweli chama hicho cha upinzani kina nia ya dhati ya kuitekeleza ajenda hiyo ni vyema wakajitokeza hadharani na kumuunga mkono Dk Magufuli, ambaye ameonesha si tu kwa kulizungumzia ajenda hiyo ya kupambana na ufisadi, bali anaitekeleza kwa vitendo.
    Dk Magufuli tangu ashike madaraka Novemba 5, mwaka huu, amekuwa kwa vitendo, akipambana na ufisadi katika kile ambacho mwenyewe alikiita ni kutumbua majipu, kwa kuwafukuza baada ya watendaji wa serikali na kuwasimamisha kazi wengine kutokana na ubadhirifu.
    Hatua yake hiyo imepongezwa na Watanzania wengi pamoja na jumuiya za kimataifa kwa jinsi anavyoshughulikia suala la kupambana na ufisadi, huku akisisitiza kuwa nia ya serikali yake ni kuwajali Watanzania wanyonge ili wafaidi rasilimali za nchi yao.
    Kuhusu kufukuzwa kwa Edward Lowassa kutoka CCM, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM alisema Lissu amekuwa akiwadanganya Watanzania, kwa kuwa Chadema inafahamu kuwa pindi walipompokea Lowassa, ndipo walipoamua rasmi kuachana na ajenda ya kupambana na ufisadi.
    “Kabla hawajamchukua, sisi tulijaribu kuwaambia kwa nini tulimkataa Lowassa, hawakutusikiliza, sasa waache kudanganya wananchi. Lowassa alipoenda kwenye chama chao ndiye aliyeua ajenda ya ufisadi,” alieleza Nape.
    Akijibu swali kwa nini CCM haikumfukuza Lowassa hadi alipoondoka mwenyewe kama ilitambua kuwa ana kasoro kiutendaji, Nape alisema chama hicho kilishaanza kuchukua hatua na ndio maana ilianzishwa operesheni ya kuvua magamba.
    “Huyu tulishaanza kushughulika naye, si lazima umfukuze mtu ndio ujulikane umeshughulikia, tulimshughulikia hadi akaondoka mwenyewe,” alieleza Nape.
    Lowassa alijiuzulu nafasi ya Uwaziri Mkuu Februari 2008, baada ya kuhusishwa na sakata la zabuni ya kampuni ya kufua umeme ya Richmond, na mwaka jana alijitosa kuwania urais ndani ya CCM, lakini jina lake lilikwama katika vikao vya uteuzi Julai.
    Mwezi mmoja baadaye alikimbilia Chadema ambako aliteuliwa kuwa mgombea urais, lakini alishindwa na Dk Magufuli.
    Hivi karibuni, Lissu alikaririwa na moja ya gazeti la kila siku (si HabariLeo) akibainisha kuwa upinzani utaendeleza ajenda ya ufisadi kwa kuwa ajenda za taifa ziko nyingi na Rais Magufuli, hataweza kuzitekeleza mwenyewe.

    Chanzo Gazeti la HabariLeo.

    0 comments:

    Post a Comment