Monday, 11 January 2016

Tagged Under:

Maalim Seif amkubali Rais Magufuli

By: Unknown On: 22:47
  • Share The Gag
  • Katibu Mkuu wa chama cha wananchi CUF Seif Sharif Hamad akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana kuhusu hatma ya uchaguzi wa Zanzibar. Kulia kwake ni Mwenyekiti wa Kamati ya muda ya Uongozi wa chama hicho.

    MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Seif Sharif Hamad, amesema ana imani na jitihada za Rais John Magufuli katika kutafuta suluhu ya mgogoro wa kisiasa visiwani Zanzibar.
    Amemtaka Magufuli aingilie kati kutafuta mbinu muafaka, inayoendana na matakwa ya kisheria na kikatiba, kumaliza mgogoro huo.
    Aidha Seif ambaye ni Katibu Mkuu wa Chama cha Waanchi (CUF) na mgombea Urais Zanzibar, alisema chama hicho hakiko tayari kurudia uchaguzi, kwa kuwa wanaamini kuwa uchaguzi uliofanyika Oktoba mwaka jana, ulikuwa huru na haki na tamko la kuufuta lilikuwa batili.
    Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, alisema tangu kufutwa kwa uchaguzi huo na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) Jecha Salim Jecha, kumefanyika vikao takribani vinane vinavyoshirikisha viongozi mbalimbali, wakiwemo marais wastaafu wa Zanzibar, Rais wa Zanzibar Dk Ali Mohammed Shein na Rais Magufuli.
    “Kwa kuwa suala hili ni kubwa na limeathiri taswira ya nchi mbele ya jamii ya kimataifa na kwa kuwa Rais Magufuli alipozungumza na waandishi wa habari baada ya kukutana na mimi (Maalim Seif) Ikulu Dar es Salaam alisisitiza haja ya kulipatia ufumbuzi wa haraka suala hili…” …”Tunaona wakati umefika yeye mwenyewe aongeze juhudi zenye lengo la kufanikisha hatua tulizopendekeza ambazo ni kuendelea kuhesabiwa kwa kura katika majimbo tisa yaliyobaki na kutangazwa rasmi kwa mshindi kupitia uchaguzi wa mwaka jana na si kurudia uchaguzi mpya,” alisema Seif.
    Kuhusu Rais Magufuli
    Alisema Rais Magufuli amefanya kazi kubwa ya kutia moyo ya kuhakikisha mazungumzo kuhusu muafaka wa uchaguzi Zanzibar, yanakamilika kwa ufanisi na kwa kuzingatia matakwa ya Katiba na Sheria.
    “ Rais John Magufuli amefanya kazi kubwa ya kututia moyo ili tukamilishe mazungumzo hayo kwa ufanisi na kwa kuzingatia matakwa ya Katiba na Sheria. Alikutana na mimi na baadaye alikutana na Dk Ali Mohamed Shein,” alisema Maalim Seif.
    Alisema “Ukweli ni kwamba katika vikao hivyo vinane bado Dk Shein na Balozi Ali Idd ambaye ni Makamu wa Pili wa Rais wameendelea kung’ang’ania kurudiwa kwa uchaguzi huku wakimtetea kwa nguvu Jecha, mimi nasisitiza haja ya kuheshimu matakwa ya Kikatiba na Kisheria na maamuzi ya wananchi wa Zanzibar” .
    Alisema anaamini kuwa Rais Magufuli kupitia mazungumzo waliyowahi kuyafanya, alionesha wazi kuwa anataka mzozo unaoendelea umalizike kwa kuhakikisha kila upande unaridhika.
    “Nadhani Dk Magufuli akiwa Amiri Jeshi Mkuu hayuko tayari kuunga mkono misimamo ambayo hapo baadaye itabidi atumie majeshi yake kutuliza ghasia. Nasisitiza I have confidence in him (nina imani naye) kwamba anataka suala hili limazikike kwa pande zote kuridhika,” alisisitiza.
    Alisema chama chake kinaamini kuwa uchaguzi visiwani humo kurudiwa si suluhisho la mgogoro uliopo bali badala ya kutuliza mgogoro uliopo, utaanzisha vurugu na fujo hasa pale wananchi watakapohisi hawatendewi haki juu ya maamuzi yao.
    Alisema uchaguzi huo haufai kurudiwa kwa sababu hakuna uhalali wa msingi unaosababisha urejewe kutokana na kile alichodai ni kitendo cha Mwenyekiti wa ZEC Jecha, kutokuwa na uhalali wa kufuta uchaguzi Kikatiba na Kisheria.
    Alisema Mwenyekiti huyo alifuta uchaguzi huo bila kushirikisha wajumbe wake ambapo kwa mujibu wa Sheria ni kosa. Aidha alisema pia chama hicho hakikubali uchaguzi huo kurudiwa kwa kuwa kiini cha mzozo uliopo kwa sasa ni uamuzi wa Jecha kufuta uchaguzi.
    “Uchaguzi ni wapigakura na si vyama au wagombea. Lazima wapigakura waridhishwe kuwa uchaguzi ulikuwa na tatizo kiasi cha kuufanya ufutwe…hadi sasa hakuna mwelekeo unaoonyesha kuna ukweli katika tuhuma za kasoro za uchaguzi,” alisema.
    Alipendekeza kuwa ili mzozo unaoendelea visiwani hapo umalizike ni vyema Mwenyekiti wa ZEC Jecha akaondoka kwenye wadhifa huo au ajiuzulu kutokana na kitendo cha kufuta uchaguzi bila kufuata taratibu.
    Aidha alipendekeza ZEC chini ya Makamu Mwenyekiti na Makamishna waliobaki kwa mujibu wa Sheria na Katiba, wamalizie kutangaza matokeo ya Urais kwa majimbo tisa yaliyohakikiwa na kumaliza uhakiki wa matokeo ya Urais kwa majimbo 14 yaliyobaki na kutangaza matokeo.
    Aidha alimtaka Rais Magufuli aongeze juhudi zenye lengo la kufanikisha mapendekezo hayo wakati uongozi wa CUF na CCM nao ufanye mazungumzo ya kukamilisha utaratibu wa kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar nchini ya mshindi atakayetangazwa.
    Akana kujitangaza Kuhusu madai kuwa alikiuka Sheria kwa kujitangaza mshindi kabla ya Tume ya Uchaguzi, Maalimu Seif alisema, haoni kama amefanya kosa kwani alichofanya ni kuchukua matokeo yaliyokwishatangazwa na wasimamizi wa uchaguzi na kubandikwa kwenye vituo vya uchaguzi.
    “Hakuna sehemu yoyote niliyojitangazia mimi Maalim Seif nimeshinda, ila nimechukua matokeo yaliyokwishatangazwa yanayoonyesha kuwa ninaongoza,” alisisitiza.
    Oktoba mwaka jana, Tume ya Uchaguzi ZEC ilitangaza kufuta matokeo yote ya Uchaguzi Mkuu visiwani Zanzibar baada ya kubainika kujitokeza kwa kasoro nyingi, zilizosababisha kukiukwa kwa sheria za uchaguzi na haki kushindwa kutendeka.
    Baadhi ya kasoro zilitajwa ni pamoja na baadhi ya vituo vya uchaguzi vya Pemba kuwa na idadi kubwa ya kura zilizopigwa kuliko idadi ya watu waliopo katika daftari la wapiga kura.
    Mara baada ya kufutwa kwa uchaguzi huo, vikao mbalimbali vilifanyika vilivyoshirikisha wagombea wapinzani katika uchaguzi huo ambao ni Seif na Dk Shein ili kuwezesha kupata suluhu.
    Serikali ilibainisha kuwa inajipanga kutaja tarehe ya kurejewa kwa uchaguzi upya visiwani humo.

    Chanzo Gazeti la HabariLeo.

    0 comments:

    Post a Comment