Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadik.
MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadiki amepiga marufuku
utoaji wa vibali vya malori ya mizigo na magari yenye uzito wa zaidi ya
tani 10 kuingia katika barabara zote zinazosimamiwa na Manispaa za jiji
la Dar es Salaam.
Barabara hizo ni zile zilizojengwa kwa kiwango cha lami na hatua hiyo
inatokana na barabara hizo kuharibika kwa kipindi kifupi kutokana uzito
jambo linaloisababishia Serikali hasara.
“Kuanzia leo katika mkoa wangu ni marufuku kutoa vibali vya magari
yenye uzito wa zaidi ya tani 10 kuingia kwenye barabara zetu, tunataka
barabara zidumu, watakaokaidi watachukuliwa hatua,” alisisitiza Sadiki.
Sadiki aliziagiza manispaa za jiji hilo kuweka alama za barabarani
zinazoonesha zuio kwa magari yote yenye uzito wa zaidi ya tani 10 kupita
kwenye barabara hizo ili wamiliki na madereva watakaokiuka agizo hilo
wachukuliwe hatua kali za kisheria.
Alikuwa akizungumza na wajumbe wa Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Dar es
Salaam kwenye kikao cha kwanza kwa mwaka 2016. Alisema manispaa za jiji
hilo zinatenga fedha nyingi kujenga barabara mpya na kufanya matengenezo
ya zilizopo lakini nyingi zinaharibiwa na malori ya mizigo.
Alisema baadhi ya magari yenye uzito wa tani 40 hudiriki kupita
kwenye barabara za huduma ama za dharura (service road), madaraja na
wakati mwingine maeneo ya waenda kwa miguu na kusababisha uvunjaji wa
kingo za barabara na milingoti ya taa za barabarani na kuongeza kuwa
vitendo hivyo vinaisababishia Serikali hasara kutokana na gharama ya
matengenezo.
Kuhusu ulinzi na usalama wa watumiaji wa barabara za jiji hilo,
ameitaka Polisi kuendelea kuchukua hatua na kufanya operesheni dhidi ya
madereva wa pikipiki (bodaboda) na bajaji wanaopitisha vyombo vyao vya
usafiri kwenye njia za waenda kwa miguu na kusababisha usumbufu na ajali
za mara kwa mara.
‘‘Ninaiagiza manispaa ya Kinondoni kuondoa wafanyabiashara wote
walioko eneo la kituo cha kuzalishia umeme Ubungo, eneo lile ni hatari
kwa usalama na maisha yao, kukaa pale ni kinyume cha sheria,’’ alisema
Sadiki.
Alisema mwaka huu Mkoa wa Dar es Salaam umetenga Sh bilioni 343.5
ikilinganishwa na Sh bilioni 266.6 zilizotengwa mwaka 2015/2016
kutekeleza ujenzi na matengenezo ya barabara katika maeneo mbalimbali ya
jiji hilo ili kupunguza msongamano wa magari.
Chanzo HabariLeo.
Thursday, 3 March 2016
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comments:
Post a Comment